Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) katika Wilaya ya Tanganyika imefanikiwa kukusanya mapato yaliyovuka lengo kwa zaidi ya asilimia 100 kwa mwaka wa fedha 2024/2025, kuanzia Oktoba 2024 hadi Aprili 2025. Hayo yameelezwa katika kikao rasmi kilichoongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika, Onesmo Buswelu, ambaye ni Mwenyekiti wa kikao, amepongeza mafanikio hayo na kuongeza kuwa ni hatua muhimu kuelekea maendeleo ya wananchi.
Akizungumza katika kikao hicho, DC Buswelu ameeleza kuwa mafanikio ya ukusanyaji huo wa mapato ni kielelezo cha uwajibikaji na ushirikiano mzuri kati ya serikali na wananchi. Amesema, "Ukusanyaji huu unaleta taswira ya chachu ya maendeleo kwa wananchi wetu, kwani mapato haya ndiyo yanayowezesha utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kijamii na kiuchumi."
Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika, Hamad Mapengo, amepongeza TRA kwa kuvuka lengo la ukusanyaji wa mapato na kuwahimiza waendelee kutoa elimu kwa wananchi kuhusu ulipaji wa kodi bila usumbufu. "Wananchi wakielimishwa vizuri, wataelewa wajibu wao na kuchangia kwa hiari maendeleo ya taifa letu," amesema Mapengo.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Tanganyika, Juma Shaban Juma, amesifu mafanikio hayo na kuwataka TRA kuendeleza ushirikiano uliopo kati yao na viongozi wa serikali, akieleza kuwa ushirikiano huo ndio msingi wa mafanikio endelevu katika ukusanyaji wa mapato.
Naye Katibu wa Mbunge wa Jimbo la Tanganyika, Said Wambari, ametoa wito kwa wananchi kulipa kodi kwa hiari bila kushurutishwa, akibainisha kuwa ni kwa njia hiyo tu serikali itaweza kuwahudumia wananchi kwa ufanisi zaidi.
Kwa upande wake Katibu wa kikao ambaye pia ni Meneja Msaidizi wa TRA Mkoa wa Katavi Bernard Peter, ameeleza kuwa mafanikio hayo yametokana na mikakati madhubuti ya uhamasishaji, usimamizi na ushirikiano mzuri na wadau mbalimbali. “Tumefanikisha ukusanyaji wa mapato kwa zaidi ya asilimia mia moja, jambo linaloonyesha utayari wa wananchi kushiriki katika maendeleo ya nchi yao,” amesema Bernard.
TONGWE - MAJALILA
Sanduku la barua: S.L.P 01 KATAVI - TANGANYIKA
Telephone: +255-252955264
Simu ya mkononi: 0754870344
Barua pepe: ded@tanganyikadc.go.tz
Copyright ©2018 Tanganyika-DC . All rights reserved.